Katika Biblia, kuna watu ambao
walifundishwa habari za Injili ya Yesu Kristo, wakazingatia mafundisho
yale. Baada ya kuyazingatia, wakaanza kuyaishi hivyo wakafanyika
WANAFUNZI wa Yesu, kweli kweli. Watu ambao hawakuwa wamejifunza habari
za Injili, walipoona jinsi wanavyoishi wale Wanafunzi wa Yesu,
walishangaa sana kwa kuwa walikuwa wanaishi sawa sawa na
walivyofundishwa, na maisha yao yalibadilika yakafanana na Kristo. Jambo
hili liliwafanya, wale wanafunzi, waitwe WAKRISTO. Walikuwa wamelivaa
Vazi la Ukristo. Ukristo ikawa ni Matokeo ya Vile mtu alivyo.
Miaka iliendelea, Watu wakiwa wanaitwa
Wakristo, kutokana na vile walivyokuwa wanaishi. Mwenendo wa maisha yao
uliwatetea na kuwatambulisha kwa jamii inayowazunguka kuwa wao ni
Wakristo. Lakini kadri miaka ilivyozidi kusonga ile hali ya mtu Kuitwa
Mkristo kutokana na alivyoishi nayo iliendelea kubadilika. Kukatokea
watu ambao pamoja na Kuitwa waKristo, lakini walianza kutenda mambo
ambayo yanatofautiana na mafundisho ya Kristo. Hali hii ilisababisha
baadhi ya watu kutumia “Ukristo” kama njia moja wapo ya kujitetea kuwa
Yeye ni “Mtu mwema”.
Katika siku zetu, hata sasa unaposoma
maneno haya, kuna mahali kuna mtu ambaye anajiita Mkristo lakini
anatenda tofauti na Mafudisho ya Kristo. Miaka kadhaa iliyopita, wakati
badiliko hili la Ukristo kutoka katika kuwa Matokeo ya mtu anavyoishi na kuwa ni Mtu anayetazamiwa kuwa hivyo, Wachungaji
wengi waliibiwa na kupoteza malizao nyingi kwa kuwa watu walikuwa
wanajitambulisha kuwa yeye ni Mkristo, kwa hiyo anahitaji msaada wa
kulala japo kwa usiku huo tu ili kesho aendelee na safari yake. Na mtu
akipewa hifadhi alikuwa anatumia mwanya huo kuiba na kutokomea kabla jua
halijachomoza. Vazi la Ukristo likawa limetobolewa tobolewa. Ikawa ni
lazima mtu avae vazi jingine ndani ya vazi hilo ili kukinga yale matundu
ya vazi la Ukristo.
Baada ya kuona hivyo, wale walioendelea
kuishi kwa kadri ya Mafundisho ya Yesu, ilibidi waweke vazi jingine
ndani ya Vazi la Ukristo. Wakawa wanaitwa kuwa Mtualiyeokoka. Kwamba
kule kusema tu ni Mkristo ikawa haitoshi tena, ni lazima kuwe na
kingine zaidi ya hapo. Wakawepo Wakristo Waliookoka. Ndani ya Wakristo
wakawepo Wakristo wanaoishi kidunia kabisa na Wale wanaoishi Kikristo.
Hivyo kukaja na Vazi jipya la “Kuokoka”.
Miaka imekwenda, huku vazi la Kuokoka
likiwa linatumika kuziba yale matundu ya Ukristo, lakini inaonekana kuwa
Vazi la “Kuokoka” nalo linaonekana Kuchakaa,na pengine tayari
limeshaanza kutoboka. Kule kusema mtu “ameokoka” nayo inakuwa tu ni mtu
anayetazamiwa kuwa hiyvo! Wengi wametapeliwa kwa jina la “kuokoka”.
Wasichana na wavulana wengi wamejikuta katika misiba ya ndoa kwa kuwa
wakati wa uchumba, mmoja wapo alivaa vazi la Ukristo lililotoboka, kisha
akavaa na vazi la ‘Kuokoka” ambalo nalo kumbe limetoboka pia….! Na
mifano mingine mingi ya yakuonyesha jinsi hali hii ilivyo.
Nimetafakari, nimewaza sana kuwa baada ya hivi vitambulisho viwili, au mavazi mawili kutobokatoboka, yaani Ukristo na Kuokoka kutokutosheleza
kuwa ni Jina la Mfuasi wa Kristo, ni jina gani jipya litafuatia baada
ya haya mawili? Ikiwa wakristo wa kwanza, waliookoka katika mapambazuko
ya Injili, walistahili Kuitwa Wakristo kwa kuwa waliishi kama Kristo
alivyofundisha, nadhani bado kuna uzuri kwa Wafuasi wa Kristo
kutambulika katika jamii inayowazunguka kwa kuwa Ni Mabalozi wa Kristo.
Je, hao wanatambulika au watatambulika kwa jina gani jingine?
Naendelea kuwaza.....
Maandiko ya rejea: Mdo 11:26; Lk 11:39; Math 23:25-28
No comments:
Post a Comment